Wednesday, 11 May 2016

MKUKUTA unalenga kupunguza Umaskini vijijini


 MKUKUTA ni neno maarufu katika jamii ya Tanzania toka ulipozinduliwa mwaka 2005. Kirefu chake ni Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini  Tanzania, MKUKUTA umeboreshwa kutoka katika Mkakati wa kwanza wa kupunguza umaskini wa uliozinduliwa Oktoba mwaka 2000 na unatekelezwa kuanzia 2005 hadi 2010.


Mojawapo ya eneo ambalo MKUKUTA umejikita ni ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini wa kipato. Eneo hili lina malengo sita likiwemo la kupunguza umaskini wa kipato kwa wanawake na wanaume wa maeneo ya vijijini. Inadhamiriwa ifikapo 2010 wanaoishi chini ya mstari wa umaskini wapungue toka asilimia 38.6 hadi asilimia 14.

Kupungua huko kutatokana na wakazi wa maeneo hayo ambao wengi wao ni wakulima wadogo vijijini endapo watajengewa uwezo wa kuongeza tija na kupata faida ndani na nje ya sekta ya kilimo. Kuwezesha kutafuta masoko ya uhakika ya bidhaa za kilimo. Kuwajengea uwezo wa kuongeza thamani mazao wazalishayo ili waweze kupata faida.

Wakazi wa sehemu hizo wajengewe pia uwezo wa kutumia raslimali zinazowazunguka na hivyo Kuongeza michango inayotokana na wanyama pori, misitu na uvuvi katika vipato vya jumuiya za vijijini. Haya yakitekelezwa vyema itakuwa ni rahisi kwa wakazi hao wa vijijini kupunguza umasikini wa kipato na hivyo kukuza uchumi.

Tangu MKUKUTA uanze kutekelezwa kumekuwepo na jitihada mbalimbali za wadau katika utekelezaji wake. Wananchi kila mahali wameanzisha vyama vya kukopa na kuweka (SACCOS). Vyama hivi vinawasaidia wananchi wenye kipato cha chini kupata mikopo inayowasaidia kuendeleza kilimo au biashara zao ndogo ndogo.

Takwimu zilizopatikana zinaonesha hadi mwaka 2007 karibu wajasiriamali wadogo wadogo 20.000 walipatiwa mikopo kutoka kwenye SACCOS mbalimbali nchini ongezeko zaidi linatarajiwa baada ya hatua ya serikali kutoa karibu bilioni moja kwa Mkoa ili kusaidia kuwakopesha wanyonge wasioweza kukopesheka na mabenki.

Kwa muda mrefu kilimo kimekuwa  kinakabiliwa na chanagamoto nyingi. Kasi ya kukua kwa kilimo ni asilimi 5 katika kipindi cha miaka mitatu  mfululizo. Hii inatoa picha inayobashiri kuimarika zaidi sekta hii iwapo mipango iliyopo itatekelezwa na kusimamiwa vizuri. Basi wakazi hao wa vijijini wanaweza kuondokana na umaskini.

Kwa upande mwingine, pato la taifa(GDP) linaendelea kuongezeka. Hii inaashiria uchumi wa nchi kukua. Mfano, mwaka 2006 Pato la taifa lilikuwa kwa asilimia 6.2. Lengo la MKUKUTA linasema ifikapo mwaka 2010 pato hilo liongezeke  na kufikia asilimia kati ya sita ana nane.

 Kumekuwepo na ongezeko la mapato ya wakazi wa vijijini katika sekta ya ufugaji. Ingawaje bado wafugaji wanafuga kizamani na kuuza mifugo yao bila ya kuongeza thamani, bado ng’ombe waliouzwa nje walifikia thamani ya shilingi za Tanzania bilioni 2.9 kiasi ambacho ni kikubwa na kinachangia kupunguza umaskini wa kipato vijijini.

Moja ya vikwazo  kufikia lengo hili ni miundombinu, katika maeneo ya vijijini hasa barabara na umeme ni kiwazo kikubwa cha juhudi za kujikwamua kiuchumi kwa wakazi wengi wa huko. Barabara zisizounganika zinakwaza usafirishaji wa mazao na kupata tija kwa wakati muafaka. Mazao mengi huozea mashambani hasa wakati wa msimu wa matunda

Umaskini wa kipato vijijini unachangiwa na wakulima kuendesha kilimo cha kujikimu kwa kutegemea mvua, uzalishaji duni, nguvu kazi haba na vitendea kazi duni ingawaje huduma za kilimo cha umwagiliaji zinaonesha kuanza kukua lakini wananchi wengi hawatumii kutokana na ubunifu mdogo na baadhi ya wanaotumia wamefanikiwa.

 Mitaji na fursa finyu ya kupata mikopo ni changamoto kwa wakazi wengi wa vijijini. Maeneo ya mijini tatizo linaonekana sio kubwa sana ukilinganisha na maeneo ya vijijini. Ndio maana MKUKUTA umeyatenga malengo ya kupunguza umaskini wa kipato kwa wakazi wa mijini tofauti na wale wa vijijini kwa vile wanahitaji mbinu tofauti.

Matumizi halisi ya nishati ya kupikia ni changamoto kwa wengi. Serikali inasisitiza nishati za umeme na gesi zitumike hasa ili kupunguza uharibifu wa mazingira kwa kukata miti ya kuni. Kwa wakazi wengi wa vijijini hili bado ni tatizo. Kutokana na gharama za nishati mbadala wengi hawaziwezi huendelea kutumia kuni na mkaa.

Hali ngumu ya maisha hasa umaskini wa kipato kwa mtu mmoja mmoja unaripotiwa kuongezeka hasa mwaka 2007. Karibu asilimia 82 ya vijana waliosailiwa katika zoezi la kukusanya maoni ya wananchi juu ya MKUKUTA walidai ugumu wa maisha unaongezeka kila siku kutokana na kukosa ajira na kupanda kwa garama za maisha.

Serikali licha ya kuwa na mikakati ya kuboresha miundombinu ya kiuchumi kama vile barabara, huduma za umeme na maji maeneo ya vijijini, ili kuchagiza maendeleo katika maeneo mengi ya nchi hasa vijijini, mikakati hiyo iende sambamba na upatikanaji wa nishati za uhakika na hasa umeme wa jua ambao utachangia kupunguza kazi za sulba.

Viongozi wanapaswa kuhamasisha wakulima vijijini kuzalisha mazao yenye faida kubwa na kuongeza upatikanaji wa nyenzo za kilimo na matumizi sahihi ya teknolojia Suala hili liende sanjari na mbinu za usimamizi wa mavuno katika kaya za vijijini na kukuza miradi inayoongeza thamani katika kilimo,uvuvi mifugo na bidhaa za misituni

Ili wakazi wa vijijini waweze kuinua kipato mkazo mkubwa uwekwe katika kuimarisha mafunzo ya stadi za maisha na ujasiriamali kwa watu wa vijijini hususani wanawake na vijana. Kwani kundi hili ndio limekuwa rikiathirika sana na hivyo wengi wao hukimbilia mijini wakidhani kuna unafuu na wengi wanaokosa elimu hiyo hupunjwa mazao na hivyo kubaki katika hali ya umaskini.

Katika lengo hili kuna mikakati kundi zaidi ya kumi na nane iwapo serikali na wadau watahakikisha mikakati kundi hiyo inatekelezwa haraka wananchi wa vijijini wake kwa waume wanaweza kupunguza umaskini wa kipato na kuvigeuza vijiji kuwa kimbilio la watu wengi kuliko ilivyo hivi sasa vijana huvikimbia kuogopa kuzama kwenye umaskini.

Yapo maeneo ambayo wananchi wake hawahitaji fedha kwa ajili ya mitaji ya kuongeza kipato lakini wanakabiliwa na umaskini wa kipato kutokana na sheria ambazo kama zingerekebishwa zingeweza kuwajengea mazingira mazuri ya kuinua hali za maisha yao Ni jukumu la serikali kupitia sheria  zenye mapungufu na kuziboresha ili kuleta mafanikio katika kuleta maendeleo kwa taifa.

Mungu ibariki Tanzania


No comments:

Post a Comment